Na Annamaria Makweba
Katika Utekelezaji wa Miradi ya ujenzi wa Vyuo vya Ufundi Stadi 64 vya Wilaya na Kimoja cha Mkoa Songwe , Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknologia imeanza kufanya ukaguzi wa Miradi hiyo ikiwa na lengo la kujiridhisha na utekelezaji wa matumizi ya fedha kwa awamu ya kwanza katika miradi hiyo.
Chuo cha Ufundi Stadi (Veta) kinachojengwa katika Kijiji cha Kisimiri Kata ya Uwiro Wilayani Arumeru ni miongoni mwa Vyuo vinavyojengwa na Serikali ya Awamu ya Sita ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambapo Naibu Waziri Elimu Mhe. Omari Kipanga amefika na kukagua ujenzi wa awali katika chuo hicho.
Katika Maelezo yake Naibu Waziri ameeleza kuwa Wizara ya Elimu inafanya ufuatiliaji wa karibu wa matumizi ya fedha na ubora wa kazi katika miradi yote inayotekelezwa, lengo ni kujiridhisha kazi iliyofanyika lakini pia kuruhusu fedha za awamu ya pili kuletwa na Mradi kuendelea kutekelezwa.
" Wizara inafuatilia miradi hii ili kuona kama ujenzi unaendana na vipimo au michoro iliyotolewa imefuatwa naweza kusema tunaangalia (Value for money) lakini tunaangalia ubora wa kazi" Alisema Kipanga.
Hata hivyo, Mkuu wa Chuo cha Ualimu Elimu Maalum Patandi Lucian E. Segesela ameeleza kuwa Mradi umefikia asilimia 90 ya ujenzi wa majengo yanayojengwa ambayo ni Jengo la Utawala, Majengo 3 ya Karakana, jengo la nyumba ya Mkuu wa Chuo, Jengo la madarasa, jengo la choo, jengo la kibanda cha Mlinzi na Jengo la kupokelea umeme.
Vilevile Diwani Kata ya Uwiro Mhe. Dauson A. Urio ameishukuru Serikali kwa kuleta miradi hii katika Wilaya kwani itasaidia kuboresha mazingira na kuongeza fursa kwa Vijana kujiendeleza na baadae kujiajiri.
Katika hatua nyingine katika Ukaguzi wa Mradi huo, Mhe. Kipanga ametoa maelekezo kwa Meneja wa TANESCO , TARURA na RUWASA Wilaya ya Arumeru kuhakikisha huduma ya Umeme, Barabara na Maji zinapatikana katika maeneo ya mradi ili kurahisisha utekelezaji wa mradi huo.
Ikumbukwe kuwa Serikali ya Awamu ya Sita imetoa shilingi Bilioni 1.6 ikiwa ni awamu ya kwanza ya utekelezaji wa Mradi wa Ujenzi wa Chuo hicho.
Halmashauri ya Wilaya ya Meru
Anwani: P.o. Box 462 Usa River
Simu ya Mezani: (+ 255) 272970482
Simu ya mkononi:
Barua pepe: ded@merudc.go.tz
Hakimiliki@2017 Halmashauri ya Wilaya ya Meru. Haki zote zimehifadhiwa