Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Meru laidhinisha rasimu ya bajeti ya mwaka wa fedha 2023/2024 kiasi cha Bilioni 54.1 ambapo kati ya fedha hizo kiasi cha Bilioni 5.31 ni mapato ya ndani ya Halmashauri.
Akizungumza wakati wa mkutano maalum wa baraza hilo,Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Meru, Mhe.Jeremia Kishili amesema rasimu hiyo ya bajeti kiasi cha Bilioni 54.1 imejikita kuwaletea wanananchi maendeleo ikiwa ni kuongeza na kuboresha miundombinu ya huduma za kijamii, ambapo katika rasimu hiyo kiasi cha bilioni 10.49 kimetengwa kama fedha za maendeleo kwa mchanganuo wa bilioni 1.3 ni fedha za maendeleo zitokanazo na mapato ya ndani na bilioni 9.19 ni fedha za maendeleo toka Serikali Kuu.
Vilevile, Mhe.kishili amebainisha Halmashauri hiyo kuendelea kukusanya mapato na kuwaletea wananchi maendeleo sambamba na kuhakikisha fedha zote zinazoletwa kwa ajili ya shughuli za maendeleo zinasimamiwa ipasavyo ili kuleta tija iliyokusudiwa ambapo amewataka wakusanya mapato ya Halmashauri kuwa waadilifu na ufanisi Mkubwa. Pia ametoa wito kwa wananchi kudai risiti kwa malipo ya tozo za Halmashauri .
Awali, akiwasilisha rasimu hiyo kwa niaba ya Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Meru, Bw.Daudi Wengi, Afisa Mipango Halmashauri hiyo ameeleza katika rasimu hiyo ya bajeti kiasi cha Bilioni 54.1, kiasi cha Bilioni 5.3 ni fedha zitokazano na vyanzo vya mapato ya ndani, kiasi cha bilioni 38.41 ni ruzuku ya mishahara, kiasi cha bilioni 1.18 ni ruzuku ya matumizi mengine na kiasi cha bilioni 9.19 ni fedha za maendeleo ya ndani na nje.
Ikumbukwe, Mpango huo wa bajeti umeandaliwa kwa mujibu wa kifungu Na. 11 cha sheria ya Sheria ya Bajeti Na. 21 ya mwaka 2015 pamoja na Kanuni zake, maelekezo na mwongozo wa kitaifa maandalizi ya Bajeti, unaoelekeza kupokea mapendekezo na vipaumbele kisekta kuanzia ngazi ya vitongoji, vijiji, kata, Idara na Vitengo vya halmashauri.
Meru Dc tupo vizuri
Halmashauri ya Wilaya ya Meru
Anwani: P.o. Box 462 Usa River
Simu ya Mezani: (+ 255) 272970482
Simu ya mkononi:
Barua pepe: ded@merudc.go.tz
Hakimiliki@2017 Halmashauri ya Wilaya ya Meru. Haki zote zimehifadhiwa