Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Meru Mhe. Jeremia Kishili amewataka watoa huduma ya Afya kutunza Siri za wagonjwa wanaowahudhumia hasa wenye maambukizi ya Virusi vya UKIMWI.
Ameyasema hayo katika Maadhimisho ya siku ya UKIMWI Dunia ambayo hufanyika kila mwaka Disemba Mosi na kwa mwaka huu 2023 Halmashauri ya Wilaya ya Meru imeadhimisha siku hiyo katika Ukumbi wa Chuo cha Mifugo Tengeru huku Kauli mbiu ikiwa ni JAMII IONGOZE KUTOKOMEZA UKIMWI.
Aidha, Mhe.Kishili Amewataka watoa huduma ya Afya kuwafuatilia wale wote wenye maambukizi ya VVU ambao hawatumii dawa waanze kutumia Dawa za kufubaza Virusi vya UKIMWI ili waweze kuishi kwa Muda Mrefu ikiwa ni pamoja na kutowanyanyapaa waathirika wa VVU.
Halmashauri ya Wilaya ya Meru imeungana na Watanzania kote nchini kuadhimisha siku ya UKIMWI Duniani ambapo Mganga Mkuu Halmashauri hiyo, Dr. Evarist Chiweka ameeleza kuwa asilimia 71% ya watu wenye maambukizi wanapata matibabu na lengo ni kuhakikisha kutokomeza maambukizi mapya hadi kufikia mwaka 2030.
Hata hivyo, katika Maadhimisho hayo, Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri ya Meru Mwl. Zainabu J. Makwinya pamoja na Viongozi wengine waliwasha mishumaa kama ishara ya kuwaombea na kuwakumbuka wale wote waliofariki kwa ugonjwa wa UKIMWI.
Kwa upande wa washiriki ambao wamejitokeza katika maadhimisho hayo, wametoa shukrani kwa idara nzima ya Afya hususani kwa Halmashauri ya Wilaya ya Meru kwani wamekuwa wakipatiwa huduma ambazo ni sahihi. Huduma zilizotolewa ni pamoja na Upimaji wa Virusi vya UKIMWI, kupima Presha na Kuchangia Damu.