Wananchi wa Kijjiji cha Kaloleni Kata ya Majengo Halmashauri ya Wilaya ya Meru, Wilayani Arumeru wamemshukuru Dkt.Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutoa Milioni 106.3 za ujenzi wa vyumba vitatu vya madarasa na vyoo vya wanafunzi wa kike matundu manne.
Wananchi wamesema hayo wakati wa ziara ya Mkuu wa Wilaya ya Arumeru Mhe.Emmanuela Kaganda ya kukagua utekezaji wa miradi ya BOOST katika Halmashauri ya Wilaya ya Meru.
Akizungumza kwa niaba ya Wananchi wa Kaloleni Diwani wa Kata ya Majengo Mhe.Bernard Kivondo amemshukuru Rais.Samia kwa kuendelea kutoa fedha za maendeleo katika shule ya Msingi Kaloleni kwa awamu ambapo Serikali kupitia TASAF ilitoa milioni 74 za ujenzi wa Vyumba viwili vya madarasa na ofisi, pia ilitoa milioni 12.5 za ukamilishaji wa boma na sasa imetoa Milioni 106.3 fedha za mradi wa BOOST kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vitatu vya madarasa na vyoo .
Aidha, Mhe.Kivondo amesema Wananchi wa Kaloleni wamehamasika na maendeleo yanayofanywa na Serikali ya Dkt.Samia Suluhu Hassan na wanashiriki kikamilifu katika utekelezaji wa miradi kwa kuchangia nguvu kazi ambapo vitongoji vya kijiji cha Kaloleni vinautaratibu wa zamu ya nguvu kazi.
Awali, Mkuu wa Wilaya ya Arumeru Mhe.Emmanuela Kaganda amesema Serikali ya Dkt.Samia Suluhu Hassan imejipanga kuwaletea wananchi wake maendeleo kwa ngazi zote ambapo katika sekta ya elimu msingi imetoa milioni 961.5 fedha za BOOST kwa ajili ya uboreshaji wa miundombinu katika shule za msingi ili kuhakikisha watoto wa Kitanzania wanapata elimu bora katika mazingira rafiki.
Aidha, Mhe.Kaganda ameelekeza miradi inayotekelezwa kuwa na viwango na ubora sambamba na kutekelezwa kwa wakati .
*Ikumbukwe*
Ilani ya CCM ya mwaka 2020, Sura ya tatu ibara ya 78 inaeleza "CCM inatambua kuwa rasilimaliwatu ndio nyenzo muhimu ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi. Aidha CCM inaamini kuwa elimu bora ndio nyenzo muhimu ya kujenga ,kulea na kuendeleza rasilimaliwatu ili ziweze kuchangia kikamilifu katika ujenzi wa Taifa na maendeleo ya jamii kwa ujumla"
Halmashauri ya Wilaya ya Meru
Anwani: P.o. Box 462 Usa River
Simu ya Mezani: (+ 255) 272970482
Simu ya mkononi:
Barua pepe: ded@merudc.go.tz
Hakimiliki@2017 Halmashauri ya Wilaya ya Meru. Haki zote zimehifadhiwa